Zoezi la uhuishaji wa taarifa za wakulima wa zao la korosho linaendelea kwa mafanikio makubwa katika ofisi za vijiji yalipo mashamba ya wakulima likiwa chini ya usimamizi wa Maafisa Kilimo walioajiriwa na Bodi ya Korosho Tanzania chini ya mpango wa Jenga Kesho Iliyo Bora (Building a Better Tommorow) BBT na viongozi wa vijiji husika.
Kwa upande wake ndg. Khamis Burian mkulima kutoka Kijiji cha Shaba kata ya Mtimbwilimbwi mkoani Mtwara ambaye tayari amehuisha taarifa zake, anasema kuwa zoezi la uhuishaji taarifa linaendelea vizuri na anaishukuru Bodi ya Korosho Tanzania kwa jitihada zake za kuwahudumia wakulima. “Bodi ya Korosho imeamua kutuboreshea zao la korosho sisi wakulima, msimu uliopita nilivuna tani sita na matarajio yangu katika msimu huu ni kuvuna tani nyingi zaidi” anaeleza ndg Khamis.
Naye Bi. Zainabu Ismail ambaye ni mkulima kutoka Kijiji cha shaba kata ya Mtimbwilimbwi mkoani Mtwara ambaye pia tayari amehuisha taarifa zake, anaeleza kuwa zoezi la uhuishaji linaendelea vizuri na ni matarajio yake kupata mavuno mengi zaidi mara baada ya kupata pembejeo za ruzuku zinazotolewa bure na serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Zoezi la uhuishaji taarifa za wakulima wa zao Korosho linafanyika kila siku za jumatatu hadi Jumamosi katika ofisi za watendaji wa vijiji yalipo mashamba ya wakulima kuanzia saa 2:00 asubuhi hadi saa 11:00 jioni. Lilianza rasmi februari 17-2025 na linatarajia kufikia tamati machi 31, 2025.