Imeelezwa kuwa jumla ya Tani 180,342 za korosho zimeuzwa katika msimu wa 2024/2025 ndani ya wiki tatu za minada ikilinganishwa na Tani 60,066 ambazo zilikuw zimeuzwa kufikia wiki ya tatu katika msimu uliopita.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi mkuu wa bodi ya korosho ndg. Francis Alfred wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mwenendo wa mauzo na soko la korosho ghafi katika msimu wa 2024/2025 hadi kufikia tarehe 30 oktoba 2024.
Pia ndg. Alfred amebainisha kuwa kwasasa wastani wa bei zilizoko sokoni ni Tsh. 3200 Kwa kilo moja ikilinganishwa na shilingi 1850 Kwa kilo katika msimu uliopita.
“Ongezeko la uzalishaji pamoja na Bei ya korosho umeleta hamasa kwa wakulima na hivyo wakulima wengi kupeleka korosho zao katika vyama vya msingi mapema ili kunufaika na bei iliyopo” ndg Alfred.
Aidha Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho ameishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoaji wa ruzuku za pembejeo kwa 100% pamoja na kuboresha masoko ya bidhaa za kilimo.