Maafisa Ugani Kilimo walioajiriwa na Bodi ya Korosho Tanzania kupitia program ya BBT Korosho waliopo Mtwara – Makao Makuu ikiwa ni moja kati ya vituo tisa vinavyotoa mafunzo, wameendelea na mafunzo ya nadharia na vitendo kama sehemu ya mwendelezo wa mafunzo yao yaliyoanza Januari 13, 2025.
Mafunzo hayo yanahusisha ufahamu wa mbinu bora za kilimo cha korosho ikiwa ni pamoja na udhibiti wa magonjwa na wadudu waharibifu kupitia matumizi sahihi na salama ya viuatilifu ili kuongeza uzalishaji wa korosho nchini.
Vile vile maafisa hawa wamepata ujuzi kwa vitendo utakaowasaidia kuhamasisha wakulima na kuwasiliana nao kwa ufanisi ili kuboresha zao la korosho.
Mafunzo hayo ni utekelezaji wa programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) iliyopo Wizara ya Kilimo katika zao la Korosho ili kuhakikisha kuwa maafisa hawa wanakuwa na uwezo wa kutoa huduma bora kwa wakulima wa korosho na hivyo kuchangia katika ukuaji wa kipato chao na Taifa kwa ujumla.