Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Patrick Sawala amesema kuwa ni matumaini yake kuwa mafunzo ya Umahiri Kwenye Mnyororo wa Thamani wa zao la korosho yanayofanyika mkoani Mtwara, yataleta tija kwa washiriki na wataalam mbalimbali kwa kuwaongezea uzoefu na kujua namna gani wengine wanafanya katika uzalishaji wao.
Kanali Sawala ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo mkoani Mtwara, yanayowakutanisha washiriki kutoka nchi nane barani Africa zinazolima na kutumia zao la korosho ambazo ni pamoja na Tanzania, Kenya, Uganda, Msumbiji, Rwanda, Ghana, Sudan Kusini, na Zambia.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania ndg. Francis Alfred amesema kuwa korosho inayozalishwa nchini Tanzania ni bora sana ukilinganisha na korosho zingine zinazolimwa katika mataifa mengine barani Africa na duniani kwa ujumla.
Ndg. Alfred amesema kuwa Bodi ya Korosho Tanzania inaendelea kudumisha ubora wa korosho inayozalishwa nchini, kwa kuendelea kufanya bidii katika kuongeza uzalishaji kufikia tani 700,000 msimu wa 2025/2026 na tani 1,000,000 ifikapo 2030.
Hayo yote yanajiri wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Umahiri Kwenye Mnyororo wa Thamani wa zao la korosho yanayofanyika mkoani Mtwara katika Ukumbi wa mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania.