Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Bodi ya Korosho Tanzania Brig. Gen. mstaafu Aloyce D. Mwanjile (ndc) ameitaka Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) kuendelea kuwaunga mkono wabanguaji nchini, kwani wana mchango mkubwa katika mnyororo wa thamani wa zao la Korosho.
Vilevile Brig. Gen. Mwanjile (ndc), ameitaka Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) kuendelea kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya viuatilifu, umuhimu wa kanzidata na mambo mbalimbali yahusuyo tasnia ya Korosho kupitia vyombo mbalimbali vya habari hasa redio za kijamii.
Ameyasema hayo wakati wa kikao cha pili cha bodi ya wakurugenzi wa CBT kilichofanyika tarehe 11 julai, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Bodi ya Korosho Tanzania mkoani Mtwara, kikiwakutanisha wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi na wajumbe wa menejimenti ya CBT.
Aidha katika kikao hicho taarifa mbalimbali zimewasilishwa ikiwamo taarifa ya usambazaji wa pembejeo za ruzuku kwa wakulima msimu wa 2025/2026 na taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kongani la viwanda uliopo katika Kijiji cha Maranje na ujenzi wa ghala, taarifa ya maandalizi ya usajili wa kampuni za usafirishaji kwa msimu wa 2025/2026 na nyingine nyingi.