Wakulima wa korosho kupitia Chama Kikuu cha Ushirika cha MAMCU wamefanikiwa kuuza jumla ya kilo 35,445,155 za korosho katika mnada wao wa kwanza uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Mji Nanyamba, mkoani Mtwara. Korosho hizo zimeuzwa kwa bei ya juu ya Sh. 2,510 na bei ya chini ya Sh. 2,310 kwa kilo.
Akizungumza mara baada ya mnada huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa TMX, Godfrey Malekano, amesema kwamba msimu huu wakulima wameimarika kwa kiasi kikubwa katika suala la ubora wa korosho zao. Ameongeza kuwa matumaini ni makubwa kuona hali ikiendelea kuwa nzuri, hatua itakayowawezesha wakulima kupata mapato zaidi kwa maendeleo yao na jamii kwa ujumla.
Kwa upande wake, Kaimu Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Mtwara, Robert Nsunza, ametoa wito kwa viongozi wa Ushirika kuhakikisha malipo kwa wakulima yanafanyika kwa wakati stahiki ili kuwaongezea imani na hamasa kwenye uzalishaji.
Hadi kufikia sasa, jumla ya korosho ghafi (RCN) zilizouzwa kupitia minada yote ni kilo 93,879,726.

