Febuari 15, 2026 05:17
Bodi ya Korosho Tanzania
Habari ZinazojiriKiteleziMatukio

WAKULIMA RUNALI WAUZA KOROSHO KILO 20,630,516 KWA BEI YA JUU TSH 2,610

Wakulima wa korosho kupitia Chama Kikuu cha Ushirika cha RUNALI, kinachounganisha wilaya za Ruangwa, Nachingwea na Liwale mkoani Lindi, wameuza jumla ya tani 20,630 za korosho ghafi katika mnada wa kwanza uliofanyika Novemba 10, 2025. Katika mnada huo, korosho zimeuzwa kwa bei ya juu ya shilingi 2,610 na bei ya chini ya shilingi 2,460 kwa kilo.

Akizungumza mara baada ya mnada huo, uliofanyika kupitia Mfumo wa Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT), Ndugu Francis Alfred, amewapongeza wakulima wa RUNALI kwa kufanikiwa kuuza korosho zao zote. Aidha, amewahimiza kuendelea kusimamia ubora wa korosho ili kuongeza ushindani na kupata masoko bora zaidi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, Mhe. Hassan Ngoma, aliwataka wakulima wa RUNALI kuendelea kuzingatia ubora ili bei ziendelee kupanda. Pia aliwasisitiza kutumia vyema mapato yao kwa maendeleo ya familia na jamii zao.

Mnada huu ni wa tatu tangu kufunguliwa kwa minada ya msimu wa 2025/2026 wilayani Tandahimba mkoani Mtwara kupitia Chama Kikuu cha Ushirika cha TANECU, na ni wa pili kufanyika mkoani Lindi baada ya mnada wa LINDI MWAMBAO.

Related posts

TANGAZO LA MAFUNZO YA UDHIBITI UBORA WA KOROSHO GHAFI MSIMU 2025/2026 KWA WADAU WA TASNIA YA KOROSHO NCHINI.

Amani Ngoleligwe

TICC EVENT PUBLIC ANOUNCEMENT

Peter Luambano

MAFUNZO YA UHUISHAJI NA USAJILI WA WAKULIMA WA KOROSHO

Peter Luambano